Skip to main content

taarifa kwa umma

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
KURUGENZI YA MAWASILIANO YA RAIS IKULU

Simu : +255-22-2114512, 2116898
Tovuti : www.ikulu.go.tz
Faksi : 255-22-2113425
OFISI YA RAIS,
IKULU,
1 BARABARA YA BARACK OBAMA,
11400 DAR ES SALAAM,
TANZANIA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 24 Agosti, 2017 amemuapisha Brigedia Jenerali John Julius Mbungo kuwa Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
Hafla ya kuapishwa kwa Brigedia Jenerali John Julius Mbungo imefanyika Ikulu Jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Kaimu Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma, Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. George Mcheche Masaju, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Anjellah Kairuki, Waziri wa Sheria na Katiba Mhe. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi na Wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama.
Pamoja na kula kiapo cha kuwa Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Brigedia Jenerali John Julius Mbungo amekula kiapo cha uadilifu kwa viongozi wa umma kilichoongozwa na Kamishna wa Maadili Mhe. Jaji Mstaafu Harold Nsekela.
Akizungumza mara baada ya kiapo Mhe. Rais Magufuli amewataka viongozi wote nchini kushirikiana katika jukumu la mapambano dhidi ya rushwa ili kuepusha madhara ya tatizo hilo katika uchumi na ustawi wa jamii.
“Ukiangalia mambo makubwa tunayopambana nayo yanasababishwa na rushwa iliyosambaa kila mahali, watumishi hewa chanzo ni rushwa, dawa za kulevya ndani yake kuna rushwa, vyeti feki ndani kuna rushwa, mikataba mibovu ndani kuna rushwa, pembejeo za ruzuku ndani kuna rushwa na huko mahakamani nako ni rushwa tu” amesisitiza Mhe. Rais Magufuli.
Mhe. Rais Magufuli ameipongeza TAKUKURU kwa kazi iliyoanza kuifanya lakini ametaka juhudi zaidi ziongezwe ili watu wote wanaojihusisha na vitendo vya kutoa na kupokea rushwa washughulikiwe kwa mujibu wa sheria.
Hata hivyo Mhe. Rais Magufuli ameelezea kutoridhishwa kwake na taratibu za uchunguzi na uendeshaji wa mashitaka ya rushwa zinavyochukua muda mrefu na ametoa wito kwa viongozi wa TAKUKURU kufanyia kazi eneo hilo ili vita dhidi ya rushwa ionekane ikizaa matunda haraka.
“Tukifanikiwa kupunguza rushwa kwa angalau asilimia 80, nchi yetu itafanikiwa kutatua matatizo mengi, na ni vema mtambue kuwa hatua hizi tunazochukua zimeanza kuwavutia wafadhili wengi na wawekezaji.
“Na mimi nikiwa kiongozi wenu nimeamua kupambana na rushwa kikwelikweli, na ninawaomba nyote mshirikiane kuondoa rushwa katika maeneo yenu ya kazi” amefafanua Mhe. Rais Magufuli.
Kabla ya Mhe. Rais Magufuli kuzungumza, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Brigedia Jenerali John Julius Mbungo ameshukuru kwa kuteuliwa kushika nafasi hiyo na ameahidi kufanya kazi kwa ushirikiano na viongozi wengine wa TAKUKURU katika mapambano dhidi ya rushwa.
Nae Kamishna wa Maadili Mhe. Jaji Mstaafu Harold Nsekela amewataka viongozi wote wa umma kuhakikisha wanajaza fomu za tamko la mali kwa wakati na pia amewataka kutoa ushirikiano kwa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma pale inapochukua hatua ya kufanya uhakiki wa taarifa zilizojazwa katika fomu hizo.
Kwa upande wake Waziri Anjellah Kairuki na Mkurugenzi wa Utawala wa TAKUKURU Bw. Alex Mfungo wamemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa kumteua Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU na wamemhakikishia kuwa wataendelea kufanya kazi kwa bidii.



Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
24 Agosti, 2017

Comments

Popular posts

Ugonjwa wasababisha Manji kutofika mahakamani

Mfanyabiashara nchini, Yusuf Manji ameshindwa kufika mahakamani kusikiliza kesi yake inayomkabili kutokana na kuwa mgonjwa. Kesi hiyo ya uhujumu uchumi imeahirishwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kutokana na mtuhumiwa huyo kutofika mahakamani hapo. Wakili wa serikali Estazia Wilson ameiambia Mahakama mbele ya Hakimu, Godfrey Mwambapa kuwa Manji hajafika Mahakamani hapo kwa vile ni mgonjwa ambapo kesi hiyo imeahirishwa hadi Agosti 25 mwaka huu itakapotajwa tena. Manji na watuhumiwa wenzake watatu wanakabiliwa na mashtaka saba yakiwemo ya uhujumu uchumi, kukutwa na mihuri miwili ya JWTZ, ukiwemo wa Mkuu wa Kikosi cha 21 JWTZ, wa Mkuu wa Kikosi Makutupora Dodoma (JWTZ) na wa Commanding Officer Korogwe na magari ya serikali. Watuhumiwa wengine katika sakata hilo ni Deogratius Kasinda na Thobias Pwere na mwingine ambaye jina lake halikufahamika mara moja, wote wamerudishwa rumande.

Mwanzo wa mwisho wa dunia utakuwa Jumatatu 21 Agosti?

Jua litapatwa na mwezi kikamilifu Amerika kaskazini kwa mara ya kwanza kabisa Jumatatu tangu 1918 Mnamo Jumatatu tarehe 21 Agosti, tukio lisilo la kawaida litashuhudiwa Amerika Kaskazini, ambalo limewavutia watu zaidi ya milioni saba wanaotarajia kulishuhudia katika miji mbalimbali Marekani. Kwa mara ya kwanza tangu 1918, jua litapatwa kikamilifu na mwezi Marekani. Bara lote la Amerika Kaskazini litafunikwa na giza totoro mchana. Ingawa baadhi ya watu wanalitazama tu kama tukio la kuvutia, kwa wengine, hili linaashiria mwisho wa dunia kama tunavyoifahamu kwa sasa. Makundi mbalimbali ya Kiinjilisti nchini Marekani kwa mfano, yameanza kuhubiri kwamba tukio hilo linaashiria kukaribia kwa mwisho wa dunia. Tovuti moja ya unabii wa Kikristo kwa jina Unsealed imedai kwamba tukio hilo la Jumatatu litaanzisha kipindi cha Majonzi, kipindi cha miaka saba ambapo katika kipindi hicho asilimia 75 ya watu wote duniani wataangamizwa. Kwa wengine hata hivyo, ni tukio ambalo wamesubiri san...