Skip to main content

Maalim Seif amlima barua msajili wa vyama vya siasa

Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad ameendelea kulia na Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi kutokana na kile alichodai ni hujuma anazozifanya dhidi ya chama hicho akishirikiana na Profesa Ibrahim Lipumba.

Maalim Seif alieleza hayo juzi katika barua yake ya kumjibu Jaji Mutungi kuhusu hatua yake ya kuwatambua Profesa Lipumba kama mwenyekiti halali wa CUF na Magdalena Sakaya kama kaimu katibu mkuu wakati viongozi hao walisimamishwa uanachama kwa tuhuma mbalimbali.

Katibu mkuu huyo alifikia uamuzi wa kumjibu Jaji Mutungi baada ya ombi lake la kuwafukuza uanachama wabunge wawili; Sakaya (Kaliua) na Maftaha Nachuma (Mtwara Mjini) kugonga mwamba kutokana na msajili kumtambua Sakaya kama kaimu katibu mkuu kufutia maelezo aliyopewa na Profesa Lipumba.

Profesa Lipumba alimweleza Msajili kuwa Maalim Seif ameshindwa kutekeleza majukumu yake ikiwa ni pamoja na kutofika ofisi ya chama hicho zilizopo Buguruni, hivyo akamteua Sakaya ambaye ni Naibu Katibu Mkuu Bara kukaimu ukatibu mkuu.

“Kwa mujibu wa katiba ya CUF mimi, Maalim Seif bado ni katibu mkuu wa chama hiki na nipo hapa nchini, ni mzima na nina akili timamu. Na nafasi yangu haiwezi kukaimiwa na Sakaya ambaye tulishamsimamisha uanachama,” inaeleza barua hiyo.

“Mheshimiwa msajili, nashangaa kwa maelezo yako. Mimi ninavyojua ni kuwa kiongozi anakaimiwa ikiwa hayupo nchini au hawezi kutekeleza majukumu yake. Hivyo ndivyo katiba ya CUF ya 1992 (toleo la 2014) kifungu cha 105 (1) kinavyoeleza.”

Aliongeza kuwa Jaji Mutungi alipokea barua ya Profesa Lipumba Machi 16, 2017 huku yeye akiwa hapa nchini akiendelea na shughuli za chama hasa katika ofisi ya makao makuu ya chama hicho iliyopo Zanzibar kwa mujibu wa katiba ya CUF.

Maalim Seif alisema cha kushangaza Msajili wa Vyama vya Siasa alitoa uamuzi kutokana na maelezo ya mwenyekiti anayetambuliwa na ofisi yake. Kutokana na hilo, mwanasiasa huyo alimtaka Jaji Mutungi kuangalia katiba ya CUF ya mwaka 1992 (toleo la 2014) kifungu Na. 1 (2) vinavyoeleza kwamba makao makuu ya chama hicho yatakuwa katika Mji Mkuu wa Zanzibar na anuani yake itakuwa kama itakavyoamuliwa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa.

Alisema kifungu cha 1 (3) kinaeleza kwamba kutakuwa na Ofisi Kuu ya Makao Makuu ya Chama Dar es Salaam na anuani yake itakuwa kama itakavyoamuliwa na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa.

“Kwa mantiki hii, Mheshimiwa Jaji Mutungi wewe mwenyewe umeshawahi kuyatembelea makao makuu hayo au bado ofisi iliyopo Buguruni, Dar es Salaam ndiyo Ofisi Kuu ya Makao Makuu?” inahoji barua ya hiyo. Maalim Seif ambaye pia aliwahi kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar, alisema kesi mbalimbali zinazohusu mgogoro wa CUF zimefunguliwa Mahakama Kuu na kwamba, ni vyema Jaji Mutungi angetumia busara kumweleza Profesa Lipumba asubiri hukumu ya mahakama na endapo angekataa msajili na ofisi yake ingejitenga naye.

Mbali na hilo, Maalim Seif alidai kwamba msajili katika barua yake alieleza kwamba amejiridhisha na maelezo ya Profesa Lipumba kuwa yeye hafiki Buguruni na ameshindwa kufanya kazi, lakini hakumtafuta au kumuita ama kumuuliza ili kupata maelezo yake kujua ukweli wa kilichoandikwa na mwenyekiti anayemtambua.   

Comments

Popular posts

Ugonjwa wasababisha Manji kutofika mahakamani

Mfanyabiashara nchini, Yusuf Manji ameshindwa kufika mahakamani kusikiliza kesi yake inayomkabili kutokana na kuwa mgonjwa. Kesi hiyo ya uhujumu uchumi imeahirishwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kutokana na mtuhumiwa huyo kutofika mahakamani hapo. Wakili wa serikali Estazia Wilson ameiambia Mahakama mbele ya Hakimu, Godfrey Mwambapa kuwa Manji hajafika Mahakamani hapo kwa vile ni mgonjwa ambapo kesi hiyo imeahirishwa hadi Agosti 25 mwaka huu itakapotajwa tena. Manji na watuhumiwa wenzake watatu wanakabiliwa na mashtaka saba yakiwemo ya uhujumu uchumi, kukutwa na mihuri miwili ya JWTZ, ukiwemo wa Mkuu wa Kikosi cha 21 JWTZ, wa Mkuu wa Kikosi Makutupora Dodoma (JWTZ) na wa Commanding Officer Korogwe na magari ya serikali. Watuhumiwa wengine katika sakata hilo ni Deogratius Kasinda na Thobias Pwere na mwingine ambaye jina lake halikufahamika mara moja, wote wamerudishwa rumande.

Mwanzo wa mwisho wa dunia utakuwa Jumatatu 21 Agosti?

Jua litapatwa na mwezi kikamilifu Amerika kaskazini kwa mara ya kwanza kabisa Jumatatu tangu 1918 Mnamo Jumatatu tarehe 21 Agosti, tukio lisilo la kawaida litashuhudiwa Amerika Kaskazini, ambalo limewavutia watu zaidi ya milioni saba wanaotarajia kulishuhudia katika miji mbalimbali Marekani. Kwa mara ya kwanza tangu 1918, jua litapatwa kikamilifu na mwezi Marekani. Bara lote la Amerika Kaskazini litafunikwa na giza totoro mchana. Ingawa baadhi ya watu wanalitazama tu kama tukio la kuvutia, kwa wengine, hili linaashiria mwisho wa dunia kama tunavyoifahamu kwa sasa. Makundi mbalimbali ya Kiinjilisti nchini Marekani kwa mfano, yameanza kuhubiri kwamba tukio hilo linaashiria kukaribia kwa mwisho wa dunia. Tovuti moja ya unabii wa Kikristo kwa jina Unsealed imedai kwamba tukio hilo la Jumatatu litaanzisha kipindi cha Majonzi, kipindi cha miaka saba ambapo katika kipindi hicho asilimia 75 ya watu wote duniani wataangamizwa. Kwa wengine hata hivyo, ni tukio ambalo wamesubiri san...